Historia

Shirika la Elimu Kibaha ni Shirika la umma linalotoa huduma mbalimbali. Shirika lipo katika Mkoa wa Pwani kilomita 40 magharibi mwa Jiji la Dar es salaam, pembezoni mwa barabara Kuu iendayo Morogoro.

Shirika la Elimu Kibaha lilianzishwa mwaka 1963 kama mradi wa pamoja chini ya wafadhili watano ambao ni Serikali ya Tanganyika kwa kipindi hicho kwa upande mmoja pamoja na nchi nne za Kinordic (Dernmark, Norway, Finland na Sweden) kwa upande mwengine. Kwa kipindi hicho mradi huu ulijulikana kama “Tanganyika Nordic Project” mpaka mwaka 1970 ambapo mradi huu ulikabidhiwa rasmi kwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na kuitwa Shirika la Elimu Kibaha. Na kusajiliwa chini ya sheria ya Mashirika ya Umma Na.17 ya mwaka 1969, marejeo ya mwaka 2002.

Kulingana na sheria ya uanzishwaji wa Shirika, Shirika la Elimu Kibaha linaongozwa na Bodi ya Wakurugenzi. Wajumbe wa bodi hiyo ni wawakilishi kutoka Wizara ya Kilimo; Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto; Wizara ya Elimu; Wizara ya Fedha na Mipango; mwakilishi kutoka OR-TAMISEMI, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha na wajumbe wengine watatu (3) watakaoteuliwa na bodi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi anateuliwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika ndiye Mtendaji Mkuu na Katibu wa Bodi hiyo, na huteuliwa na Waziri mwenye dhamana husika ya kulisimamia Shirika ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI).