Habari

SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA KUHAKIKIWA ILI KUWEZA KUPATA FEDHA ZA MRADI KUTOKA UNDP



SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA KUHAKIKIWA ILI KEWEZA KUPATA FEDHA ZA MIRADI KUTOKA UNDP 

Kibaha 10  Septemba , 2015

Shirika la Elimu Kibaha ni miongoni mwa Taasisi za Serikali nchini Tanzania ambazo baada ya kufanyiwa tathmini watanufaika na fedha za miradi kutoka UNDP. Hayo yameelezwa na Mkurugenzi  Mtendaji wa Shirika la Elimu Kibaha Dkt. Cyprian Mpemba katika kikao cha Menejimenti kilichofanyika tarehe 10  Septemba ,2015 katika ukumbi wa mikutano wa Shirika la Elimu Kibaha.

Dkt. Cyprian Mpemba amefafanua kuwa baada ya kufanyiwa tathmini na kukidhi vigezo vilivyowekwa Shirika la Elimu kibaha litanufaika kwa kupata fedha kwa ajili ya miradi mbalimbali itakayokuwa ikifadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Ameeleza kuwa tathmini hiyo itafanywa na kampuni ya EVK kwa niaba ya kampuni iliyopewa zabuni ya kutathmini taasisi zitakazokuwa na uwezo mkubwa wa kutumia fedha kutoka UNDP. Amefafanua kuwa  uadilifu, uwezo na  utoaji wa  taarifa sahihi ya matumizi ni mojawapo ya vigezo vya kuendelea kupokea fedha kutoka taasisi hiyo kubwa ya kimaendeleo duniani.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka kampuni ya EVK bw.Ephraim Kimario ameeleza jinsi tathmini hiyo itakavyofanyika. Alitaja maeneo ambayo wataangalia ikiwemo,jinsi fedha za miradi zinavyotumika , uwepo wa  watumishi wa fedha wa kutosha katika miradi hiyo ,kufuatwa kwa miongozo ya fedha  ,Ukaguzi wa ndani na wa nje kama unafanyika, utoaji wa taaarifa na tathmini ya kazi (M : E),mifumo ya Tehama kama inatumika na taratibu za ugavi kama zinafuatwa.

Shirika la maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) limekuwa likifadhili miradi ya maendeleo nchini katika Sekta za Elimu,miundo mbinu,mazingira, miradi ya wanawake na watoto na katika maeneo mengine ya kimaendeleo.