Habari

KOREA YAISAIDIA SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA


KOREA YAISAIDIA SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA

  • Ni vifaa vya tiba ya macho kwa ajili ya hospitali ya tumbi

 Kibaha – 24, Agosti,2015


Shirika la Elimu Kibaha limepokea msaada wa vifaa tiba na dawa kwa ajili ya macho kutoka Serikali ya  Korea ya Kusini kupitia Kanisa la Pool of Sloam la nchini humo. Vifaa hivyo vyenye thamani ya Sh milioni 800 ni kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani, Tumbi. Akipokea msaada huo Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Bw, Annath Nnko ameishukuru Serikali ya Korea Kusini kwa msaada huo wa mashine za kisasa vya kupima macho na vifaa kwa ajili ya upasuaji na dawa.

Kwa upande wake Bolozi wa Korea Bw. Jung Il nchini Tanzania amesema kuwa anaamini msaada huo utasaidia sana kutatua tatizo la magonjwa ya macho Mkoani Pwani. Amesema anatambua juhudi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania kuiinua nchi kimaendeleo na kwamba hata Korea ya Kusini hapo zamani walikuwa katika hali duni kiuchumi . Misaada mbalimbali na juhudi binafsi zimeifikisha nchi hiyo katika hali bora zaidi kiuchumi na hivyo anaamini Tanzania itafikia katika hali bora zaidi kiuchumi ikizingatiwa kuwa ina demokrasia pana zaidi.

Mapema akikaribisha ugeni huo Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani bwana Shangwe ,ameishukuru Serikali ya Korea ya kusini hasa Hospitali ya Sloam. Amesema kuwa anaamini msaada huu utatatua tatizo la macho linalowakabili watu wengi wa Mkoa wa Pwani .Amesisitiza kwamba technolojia itakayotumika kwa ajili ya tiba ya macho ni mpya  hivyo ni vyema pawepo mpango mzuri wa kuiendeleza technolojia hii.

Msaada huu umeambatana na  timu ya madaktari bingwa 26 wa macho kutoka Korea Kusini ambao watatoa huduma ya tiba ya macho kwa kujitolea kwa muda wa wili moja. Timu ya madaktari hao inaendelea kufanya kazi ya kutibu wagonjwa wa macho na kufanya upasuaji ambapo wagonjwa zaidi ya 100 wanatarajiwa kutibiwa.Hospitali ya Tumbi inategemewa sana na wakaazi wa Mkoa wa Pwani hasa wanaopata ajali za barabarani.