Habari
MAHAFALI YA WAHITIMU WA KIDATO CHA NNE KWA MWAKA 2018 SHULE YA SEKONDARI KIBAHA YAFANA

MAHAFALI YA WAHITIMU WA KIDATO CHA NNE KWA MWAKA 2018 SHULE YA SEKONDARI KIBAHA YAFANA
- KATIBU MKUU TUGHE AWA MGENI RASMI
Tarehe: 28,Septemba ,2018
Mahafali ya Kidato cha nne kwa mwaka 2018 yamefana ,mahafali hayo yamefanyika katika ukumbi wa B. Merlin wa Shirika la Elimu Kibaha ambapo wanafunzi 109 walitunukiwa vyeti na zawadi mbalimbali kwa waliofanya vizuri katika taaluma ,nidhamu na michezo.
Mgeni rasmi wa Mahafali hayo alikuwa ni Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa bw. Henry Mkunda ambaye aliwapongeza walimu, wazazi , Kamati ya shule, Bodi ya Shule na Uongozi wa Shirika la Elimu Kibaha kwa kuiwezesha Shule ya Sekondari Kibaha kuwa ya kwanza kitaifa katika mitihani ya Kidato cha sita kwa mwaka 2018.
Pia bw. Mkunda amewaasa wahitimu wa kidato cha nne 2018 wajiandae kwa bidii ili waweze kuwa wa kwanza kitaifa katika mitihani ya kidato cha nne inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha bw. Anathe Nnko ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Maendeleo ya Jamii aliweka mapatano na wahitimu hao wahakikishe kila mmoja wao anapata “division one” ya pointi saba.
Awali akitaja mafanikio ya Shule Mkuu wa Shule ya Sekondari Kibaha bw. Chrisdom Ambilikile ameushukuru Uongozi wa Shirika la Elimu Kibaha kwa usimamizi na kuhakikisha Shule yake inapata rasilimali za kutosha mpaka Shule imepata mafanikio mazuri kitaifa .
Pia ameshukuru Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na kiongozi mahiri Dkt. John Pombe Maghufuli kwa kuanza ukarabatii wa shule kongwe ikiwemo Sekondari ya Kibaha. Sherehe hizi zilipambwa na maonesho ya taaluma ,gwaride la skauti ,nyimbo,maigizo na muziki wa dansi.
Mgeni rasmi aliwachangia wahitumu jumla ya shilingi milioni moja baada ya kuguswa na risala ya wahitimu hao iliyoeleza kuna changamoto ya fedha kiasi cha sh milioni nne na nusu kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa uzio wa Shule. Pia aliwezesha kuwepo kwa harambee ya wazazi ambao walichangia shilingi laki tatu kwa ajili ya uzio.
TUGHE ni wadau wakubwa wa Shule ya Sekondari Kibaha ambapo awali walichangia nguzo 100 zilizogharimu shilingi milioni mbili kwa ajili ya ujenzi wa uzio wa Shule.