Habari

SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA LAPEWA SIFA ILIYOTUKUKA


SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA LAPEWA SIFA ILIYOTUKUKA

Na Lucy Semindu    -Kibaha

Tarehe 30 Septemba, 2017

Shirika la Elimu Kibaha ina sifa iliyotukuka hayo yamesemwa leo na Rais mstaafu wa Serikali ya awamu ya nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete wakati wa mahafali ya Hamsini ya Shule ya Sekondari Kibaha yaliyofanyika katika viwanja vya michezo vya Shirika la Elimu Kibaha.

Dkt. Kikwete amepata heshima kubwa ya kuwa mgeni rasmi ikizingatiwa aliwahi kusoma katika Shule ya Sekondari Kibaha ambapo amewatunuku vyeti na kuwapatia zawadi wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kibaha .

Pia alipata fursa ya kutembelea katika Bweni la Scandia E. na aliweza kuwaonesha watu waliokuwa katika msafara mahali alipokuwa analala katika bweni hilo.

Aidha , Dkt. Kikwete alipata fursa ya kukagua maonesho ya taaluma pamoja na kushuhudia jinsi Skauti wa Kibaha Sekondari walivyo wakakamavu. Amesifiu juhudi zinazofanywa na Shirika la Elimu Kibaha za kuhakikisha Kibaha sekondari inakuwa na hadhi ile ile ya kitaaluma kiasi cha mwaka 2016 kuwa Shule ya kwanza kwa Shule za Serikali katika mitihani ya kidato cha nne.

Pia ameagiza katika maktaba ya Shirika la Elimu Kibaha vipatikane vitabu vitakavyowapa elimu ya ziada wanafunzi na kwamba vitabu vya kawaida vya masomo viwepo shuleni ambapo kila mwanafunzi ataweza kuvisoma.

Pamoja na hayo ameahidi kuweka pamoja jitihada zake na za watu aliowahi kusoma nao  pamoja katika kuchangia ukarabati wa Shule ya  Sekondari ya  Kibaha ambayo imetoa viongozi wengi ambao wapo Serikalini na katika Vyuo Vikuu mbalimbali nchini Tanzania. Shule ya Sekondari Kibaha kwa sasa ina zaidi ya miaka hamsini.